Tuesday 16 December 2008

HABARI NDIO HIYO

Jamani leo nimesoma news moja inayotoa matumaini kwenye utafiti wa dawa ya ukimwi. Wanasayansi huko Pennsylvania Marekani wameweza kupunguza idadi ya virusi ndani ya nyani vinavyofanana na vya ukimwi vijulikanavyo kama simian immunodeficiency virus(SIV). SIV ni virusi vya ukimwi lakini vinazuru wanyama tuu na sio binadamu. Wanasayansi hao wameweza pia kuongeza maisha ya nyani huyo aliyekuwa ameathirika na ukimwi. Wanasayansi hayo wamefanikiwa kufanya hivyo baada ya kuziba receptor molecule ijulikanayo kama Programme Death-1 (PD-1) ambayo huzuia kazi kwa immune system yetu ipiganayo na virusi vya ukimwi. Kwa kuziba hiyo PD-1, kunachochea cells za ulinzi wa mwili (CD8 T cells) zipigane na wadudu wa ukimwi na hivyo hupunguza idadi ya kuzaliana kwa wadudu hawa. Kwa habari zaidi bonyeza hapa

Jamani habari ndio hiyo....will keep you updated.

Kumbuka UKIMWI BADO UPO.

Monday 8 December 2008

JE, DAWA ZA UKIMWI ZA KUONGEZA MIAKA YA KUISHI, ZINACHANGIA KATIKA KUAMBUKIZWA KWA WATU ZAIDI?

Sijui wewe unaonaje kuhusu hili swala. Juzi nilikutana na mtu ambaye katika mazungumzo juu ya ukimwi na maambukizo aliniuliza swali hili; "Dada hauoni kwamba madawa ya ukimwi yanasaidia kuongezeka maambukizo"? Akimaanisha kwamba watu wanaotumia madawa haya huongezewa miaka ya kuishi na kwa kufanya hivyo inaongeza namba ya wanaoambukizwa kila siku endapo watu hawa wataendelea kuwa na mahusiano ya kimapenzi na wengine wasioathirika. Sana sana Afirika, hakuna sheria yeyote ile inayomsitisha mtu mwenye ukimwi kumuambukiza kwa makusudi mwingine asiyeathirika.

Mimi naona madawa yanatengenezwa kwa madhumuni ya kuponyesha na kukinga magonjwa kwa wale walioambukizwa na kwa wasioambukizwa. Watu hawa ambao wanatumia madawa haya hupewa miaka zaidi ya kuishi, na haihusiani kabisa na kuongezeka kwa ugonjwa huu. Wale wanaoambukiza wengine kwa makusudi wanatakiwa kuchukuliwa sheria. Sijui wanajamii mnaonaje kuhusu suala hili.

Tuesday 2 December 2008

KUTENGWA NA HOFU JUU YA WATU WENYE UKIMWI, INASAIDIA KUONGEZEKA KWA MAAMBUKIZO

Ndugu mtanzania, sijui wewe unaonaje kuhusu hili swala la kuwatenga, kuwatusi, kuwashusha, na kutothaminika kwa watu wenye virusi vya ukimwi. Hii kwa lugha ya kabila jingine wanaita "HIV/AIDS Stigmatism" . Hii inatokana na tabia, mazoea, imani, sera za watu juu ya wale walioambukizwa na ukimwi, pia juu ya ndugu, marafiki, jumuia au watu wa karibu wa mtu aliyeambukizwa na ukimwi. Hii inatokana na vitu vifuatavyo:

  • Kwanza, watu wenye maambukizo haya ya ukimwi hulaumiwa kwa kupata ugonjwa huo, na watu wengi huamini kwamba yule aliyeambukizwa angeweza kuepukana na ugonjwa huo kama angefanya maamuzi mazuri.
  • Pili, ingawa ugonjwa huu una madawa ya kusaidia virusi hivyo visisambae mwilini kwa haraka, lakini hakuna matibabu ya kuviua kabisa.
  • Tatu, kuna ufinyu wa kotojua njia ya usambazwaji wa virusi vya ukimwi mwilini, na hii inawafanya watu wengi watishwe zaidi na gonjwa hili.

Hofu juu ya watu wenye ukimwi inasababishwa na watu ambao wanaiacha ikue ndani ya mioyo yao kutokana na uoga wao wenyewe. Hofu juu ya ukimwi/virusi inajibainisha yenyewe kwa njia tofauti kama, kumfukuza mtu kazi, nyumbani, au hata kuonewa kwa sababu umegundua ana ukimwi.

China na UNAIDS, wamekemea suala la hofu na kutengwa kwa watu wenye ukimwi. Kwamba kama watu walioathirika na ukimwi wasingetengwa na kudhalilishwa, na ugonjwa huu uonekana ni kama ugonjwa wa cancer au magonjwa mengine, hii ingesaidia kuwafanya watu wengi zaidi kwenda kupima na kuanza matibabu mapema. Kutengwa na kutothaminiwa kwa watu walioathirika inawezekana ndio inawapa hasira waathirika hawa na kuwafanya walipize kisasi kwa kuchukua maamuzi ya kuusambaza ugonjwa huu.

Je mdau unaonaje hili swala, je ni kweli watu wanasambaza ukimwi kutokana na kutengwa na kutothaminiwa na jamii.

Naomba maoni yenu.

Monday 1 December 2008

JE UNAJUA UNAWEZA KUTOMUAMBUKIZA MTOTO UKIMWI AKIWA TUMBONI

Mpaka sasa watu wengi wanajua kwamba inawezekana kuzuia kumuambukiza mtoto ukimwi toka kwa mama wakati angali bado tumboni. Lakini je ni wajawazito wangapi Tanzania walioathirika na ukimwi wana uwezo huo wa kununua dawa ili kukinga watoto wao wasiambukizwe?. Matokeo yake kadili ya watoto 500,000 wana maambukizo ya ukimwi kila mwaka. Blog hii ya ukimwi na mimi leo hii, siku ya ukimwi duniani inahamasisha jamii yetu, kuiomba serikali yetu ya Tanzania kuangalia jinsi ya kusaidia wakina mama wajawazito na kuimarisha PMTCT (Preventing Mother To Child Transmission).

Maambukizo haya kwa mtoto yanaweza kutokea katika kipindi cha mimba, uchungu, kuzaa ama wakati wa kunyonyesha. Bila matibabu kadilia ya asilimia 30% ya watoto huzaliwa na maambukizo katika kipindi cha mimba au kuzaa, na karibu asilimia 20 ya watoto huambukizwa kwa njia ya kunyonyesha.

Tafadhali bonyeza kwenye hii link ina maelezo mengi mazuri yanaweza kusaidia: http://www.avert.org/motherchild.htm.

SIKU YA UKIMWI DUNIANI, JE UKO SALAMA?

leo ningependelea kuwakumbusha watanzania umuhimu wa kutumia CONDOMS ili kujiepusha na magonjwa ya zinaa haswa UKIMWI. Hii ni kwa sababu leo ni siku ya ukimwi duniani na ningependa wote tuungane na watu wote duniani kuwakumbuka ndugu jamaa na marafiki waliokufa kutokana na gonjwa hili ambalo bado halijatafutiwa ufumbuzi. Kumbukumbu hii ituelimishe na kutupa tahadhari juu ya ukimwi.

UNAIDS inakadilia kwamba mpaka sasa kuna watu milioni 33.2 duniani wanaoishi na virusi vya ukimwi, kati ya hao milioni 2.5 ni watoto. Pia wanakadilia watu milioni 2.5 wameathirika kwa kipindi cha mwaka 2007 tuu. Nusu ya watu wanaoishi na ukimwi duniani ni vijana waliopata maambukizo hayo wakiwa chini ya miaka 25, na hufa kabla ya kufikia miaka 35. Karibu asilimia 95 ya watu wenye ugonjwa wa ukimwi/virusi vya ukimwi wanaishi kwenye mataifa ya kimasikini duniani, lakini virusi vya ukimwi leo ni tishio kwa watu wa jinsia zote na watoto duniani kote.

Siku ya ukimwi duniani ilianza tarehe 01/12/1988, naomba watanzania wenzangu tuelimike kuhusu ukimwi na tujue kwamba ukimwi bado upo na unaweza kunipata mimi, wewe na yule. Watanzania safari bado ni ndefu.